Category: Katiba

katiba ya zanzibar

Historia ya Katiba Yetu

Kwa mujibu wa wataalamu wa sheria kutoka chuo cha sheria cha Tanganyika(Law School of Tanganyika) Tanzania, katiba inahitaji kupitiwa mara kwa mara kuhakikisha kua inaakisi era za kidiplomasia pamoja na kwenda na wakati. Katiba ikigundulika(kwa minajili ya mapekuzi na machunguzo yakinifu) kuwa haikidhi mahitaji hayo au ikibainika kuwa ina mapungufu tume maalumu ya wataalamu wa sheria(law scholars) huundwa ili kupitia na kuirejeza kwenye ukisasa(relevance restoration).

Katiba ya Uhuru

Katiba ya Tanganyika ya mwaka 1961 ilitokana na azimio la sheria ya uhuru (Order in Council) lililopitishwa katika Bunge la Uingereza na kuletwa Tanganyika kama Katiba ya awali. Katiba hii ilitengenezwa na waingereza nchini Uingereza na kuletwa kwetu. Hata hivyo Katiba hii ilikuwa na mapungufu kadhaa kubwa ikiwa mambo mengi ya kutegemea kufanyiwa maamuzi toka Uingereza chini ya Malkia ambaye ndiye alikuwa mkuu wa nchi yetu.

Katiba ya Jamhuri

Utengenezaji wa katiba hii haukuhusisha wananchi wa kawaida. Ushiriki ulibaki mikononi mwa wabunge 71 wa TANU ambao walijigeuza na kuwa bunge maalum la Katiba lililopitisha Katiba hii. Katiba ya 1962 ndiyo ilianzisha mfumo wa Urais wa kifalme ambaye pia alikuwa Mkuu wa nchi, Amiri Jeshi Mkuu na kiongozi wa serikali. Baraza la Mawaziri na waziri mmojammoja sasa waliwajibika kwa Rais badala ya bunge.

Katiba ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar

Hii ndiyo Katiba ya kwanza ya Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar. Katiba hii ilitokana na hati za makubaliano ya muungano ambazo zilifikiwa kuelekea siku ya muungano ulifanyika tarehe 26 Aprili 1964. Katiba hii ilianzisha mambo 11 ya Muungano ambayo kwa sasa yamefikia 22. Katiba ya Tanganyika pamoja na Tanganyika yenyewe vilikufa kifo cha kawaida wakati wa kuanzisha muundo wa serikali mbili. Rais wa Zanzibar alikuwa pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano na mjumbe wa Baraza la mawaziri. Katiba hii ilianzishwa kwa tamko la Rais na kuridhiwa na bunge la Tanganyika na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. Hii ilitazamiwa kuwa Katiba ya muda ya Muungano ambayo ingetumika kwa mwaka mmoja tu na iliweka utaratibu wa kuandaa Katiba ya kudumu ya Muungano kwa kuunda Tume ya Katiba na bunge la Katiba ili kuhakikisha ushiriki wa wananchi wa Jamhuri ya Muungano unakuwepo. Tume hii ndiyo ya kwanza ya Katiba ya Tanzania na ilikuwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rashid Mfaume Kawawa.

Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Katiba hii ilijulikana kama Katiba ya mpito na ndiyo iliyorasimisha nchi kuwa ya chama kimoja cha siasa. Hata hivyo kulikuwa na vyama viwili. Tanganyika iliongozwa na Tanganyika African National Union (TANU) wakati Zanzibar ikiwa chini ya Afro Shirazi Party (ASP). Katiba ya chama cha TANU ilikuwa sehemu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jambo hili nalo limezua mjadala miongoni mwa wananchi. Katiba hii ilitokana na mchakato wa Tume ya Rais ya Katiba iliyokusanya maoni ya baadhi ya wananchi. Ghafla, mambo ya Muungano yalianza kuongezeka na utata wa uhuru (autonomy) wa Zanzibar nao ukazidi jambo ambalo limeendelea kutatiza muungano hadi sasa.

Katiba ya Kudumu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Hii ilikuwa ni Katiba ya tatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katiba hii ilipatikana kupitia Tume ya Rais iliyokuwa na wajumbe 20 (10 toka kila upande wa Muungano) ikiongozwa na Sheikh Thabit Kombo na Katibu wake akiwa Ndugu Pius Msekwa. Tume hii ilianza na kazi ya kutunga Katiba ya CCM ambayo ilizaliwa baada ya kuunganisha vyama vya Tanganyika African National Union (TANU) na Afro-Shirazi Party (ASP) tarehe 5 Februari977. Katiba yenyewe ilijikita katika misingi mikuu mitatu ambayo ni Urais wa kifalme, mfumo wa chama kimoja cha siasa na muundo wa serikali mbili. Katiba hii ilipitishwa na bunge maalum lililoteuliwa na Rais kutokana na bunge la kawaida. Kwa ujumla Katiba ya mwaka 1977 imefanyiwa mabadiliko mara 14 tangu ilipopatikana. Hata hivyo mengi ya mabadiliko hayo yamewakwepa wananchi isipokuwa yale ya 1983-1984 ambayo angalau yaliwashirikisha wananchi kwa kiasi fulani. Katika marekebisho hayo, NEC ilianzisha mjadala wa wananchi uliodumu kwa mwaka mmoja badala ya kufanya maamuzi yenyewe.

Tume ya Francis Nyalali

Rais Ali Hassan Mwinyi aliteua Tume ya kuangalia mfumo bora wa siasa nchini ikiongozwa na Marehemu Jaji Mkuu Francis Nyalali. Tume hiyo ilifanya kazi nzuri sana ikisafiri nchi nzima kukusanya maoni ya wananchi. Kutokana na kazi yake Tume ilipendekeza mambo kadhaa ikiwemo haja ya kufutwa kwa sheria 40 kandamizi. Aidha, Tume ilipendekeza kuzifanyia mabadiliko makubwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar. Mengi ya mapendekezo ya Tume hii hayakukubaliwa na Serikali isipokuwa pendekezo kuu la kuachana na mfumo wa utawala wa chama kimoja cha siasa kwenda kwenye mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Mabadiliko ya Kwanza

Madiliko haya yalifanyika miaka miwili tu baada ya kuandikwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977. Jambo kuu katika mabadiliko haya ni kuanzishwa kwa Mahakama ya Rufani inayofanya kazi katika Jamhuri yote ya Muungano.

Mabadiliko ya Pili

Mabadiliko haya yalikuja kama sehemu ya kujaribu kushughulikia kero mbalimbali za muungano. Lengo lilikuwa kujibu baadhi ya maswali yaliyokuwa yakiibuka toka Zanzibar. Ilitarajiwa kuwa marekebisho haya ya pili ya Katiba yangesaidia kuimarisha muungano jambo ambalo kwa bahati mbaya halikutokea na kupelekea marekebisho mengine mwaka huohuo.

Mabadiliko ya Tatu

Mabadiliko haya yalikuja kama sehemu ya kujaribu kushughulikia kero mbalimbali za muungano. Lengo lilikuwa kujibu baadhi ya maswali yaliyokuwa yakiibuka toka Zanzibar. Ilitarajiwa kuwa marekebisho haya ya pili ya Katiba yangesaidia kuimarisha muungano jambo ambalo kwa bahati mbaya halikutokea na kupelekea marekebisho mengine mwaka huohuo.

MABADILIKO YA TATU

Mabadiliko haya ni ya pili katika mwaka huohuo wa 1980. Kitaaluma, hii huwa ni dalili ya katiba mbovu. Mabadiliko haya yalikuja kuweka sawa mfumo wa uchaguzi wa Rais wa Zanzibar, mfumo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na muundo wa Baraza la Wawakilishi.

MABADILIKO YA NANE

Mabadiliko haya yalikuja wakati kukiwa na vuguvugu la mabadiliko kidunia kuelekea demokrasia ya vyama vingi. Mabadiliko ya nane yalifuta rasmi mfumo wa chama kimoja nchini na kuanzisha mfumo wa vyama vingi vya siasa. Aidha muundo wa bunge la muungano ulibadilika na kuanzisha viti maalumu vya wanawake kufikia asilimia 15 na viti vitano (5) toka Baraza la wawakilishi. Uandikishaji wa vyama vya siasa na uteuzi wa wagombea kupitia vyama vya siasa ulianzishwa na mabadiliko haya.

MABADILIKO YA TISA

Miezi sita baada ya mabadiliko ya nane, mabadiliko mengine yalifanywa kurekebisha utaratibu wa uchaguzi wa Rais wa Muungano, kutamka kuwa Rais anaweza kuondolewa kwa kura ya bunge kutokuwa na imani naye, kuanzisha nafasi ya Waziri Mkuu kikatiba na namna ya kumwondoa kwa kura ya kutokuwa na imani naye pia.

MABADILIKO YA KUMI

Mabadiliko haya yalikuja kuhamisha chaguzi za madiwani kuweza kufanyika pamoja na uchaguzi wa Rais na Wabunge. Pia, mabadiliko haya yaliipa mamlaka Tume ya Taifa ya uchaguzi (NEC) kusimamia chaguzi hizo.

MABADILIKO YA KUMI NA MOJA

Mabadiliko haya yalikuja wakati nchi ikijitayarisha kwenda kwenye Uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi vya siasa mwaka 1995. Mapendekezo ya mabadiliko haya yalitokana na ushauri wa Tume ya Jaji Mark Bomani ambayo ilipendekeza kuwepo kwa mgombea mwenza wa Urais wa Jamhuri ya Muungano. Mgombea mwenza huyo angekuwa ndiye Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuanzia hapo, Rais wa Zanzibar aliacha kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano lakini alibaki kwenye Baraza la Mawaziri kama mjumbe tu.

MABADILIKO YA KUMI NA MBILI

Mabadiliko haya yalipitishwa mwishoni mwa mwaka 1995 kabla ya bunge kuvunjwa rasmi na kuruhusu uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi. Aidha mabadiliko haya pia yaliweka kiapo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano na Makamu wake, Waziri Mkuu na Rais wa Zanzibar kula kiapo cha kulinda muungano. Mabadiliko haya pia yaliweka ukomo wa Rais kuwa vipindi viwili vya miaka mitano mitano.

MABADILIKO YA KUMI NA TATU

Mabadiliko haya yalikuja baada ya uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi nchini Tanzania. Kwanza, kwa mara ya kwanza Rais anaweza kuchaguliwa na kutangazwa mshindi kwa kupata kura zozote zile ili mradi awazidi wengine. Kabla mabadiliko haya, Mgombea urais asingeweza kutangazwa bila kupata angalau asilimia 51% ya kura zote zilizopigwa. Kwa sasa, hoja ni wingi wa kura tu na hivyo kuondoa uwezekano wa kura kurudiwa. Pia, mabadiliko hayo yalimpa Rais uwezo kuteua watanzania 10 kuwa wabunge wa Jamhuri ya Muungano. Aidha, mabadiliko hayo pia yaliongeza viti maalum vya wanawake toka 15% hadi 20%

MABADILIKO YA KUMI NA NNE

Mabadiliko ya mwaka 2005 yaliongeza viti maalum vya wanawake kutoka 20% hadi asimilia 30. Pia, mabadiliko haya yaliweka bayana zaidi uhuru wa kuabudu, uhuru wa kushiriki na watu wengine, uhuru wa maoni na kujieleza na kuondoa vizuizi vyote vilivyokuwepo kwenye Katiba. Kingine ni kwamba mabadiliko haya yaliweka utaratibu wa kuteua wabunge wa viti maalum vya wanawake kutegemeana na uwiano wa ushindi wa kila chama katika kura za ubunge majimboni

Read More
msaada-wa-kisheria

Isemavyo sheria ya msaada wa kisheria, 2017

Chimbuko la sheria hii lilitokana na uhitaji mkubwa wa kuwa na sheria nchini itakayoongoza kisheria namna ya utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria kwa wahitaji ili waweze kufikia haki. Sheria hii ilitungwa na bunge mnamo tarehe 31 Januari, 2017, ikapitishwa rasmi na kusainiwa na mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 21 Februari, 2017. Ilitanganzwa kwenye gazeti serikali namba 9 la 2017 na kuanza kutumika rasmi tarehe 1 Julai, 2017 kwa mujibu wa tangazo la serikali namba 20 la mwaka 2017. Pia sheria hii imetungwa kukidhi matakwa ya mikataba mbalimbali ya kimataifa ambayo nchi yetu imesaini na kuridhia kuhusu haki za binadamu ikiwemo haki ya kupata msaada wa kisheria.

“Mtu anayesaidiwa” maana yake ni mtu anayepatiwa msaada wa kisheria chini ya sheria hii.
“Mtu asiye na uwezo” Maana yake mtu asiye na uwezo wa kumudu gharama za wakili wa kujitegemea ikiwa ni pamoja na makundi mengine ya watu kama itakavyohitajika kwa maslahi ya utoaji haki.
“Ushauri wa Msaada wa kisheria” Maana yake ni ushauri na msaada unaotolewa kwa mtu asiye na uwezo katika mashauri ya jinai na madai kuhusu sheria husika, taratibu za kisheria na uandaaji wa nyaraka za kisheria.
“Msaada wa kisheiria” au “huduma ya msaada wa kisheria”inajumuisha utoaji wa ushauri wa kisheria, usaidizi wa kisheria au uwakilishi kwa watu wasiokuwa na uwezo.

“Mtoa huduma wa msaada wa kisheria” Maana yake ni taasisi iliyosajiliwa chini ya sheria hii kutoa huduma ya msaada wa kisheria.

Sheria hii imeanzisha vyombo viwili vya uratibu.

(a)Bodi ya Taifa ya Ushauri ya Msaada wa kisheria ambayo inaundwa na wajumbe wafuatao kwa kuzingatia uwakilishi wa kijinsia. Muda wa kukaa madarakani kwa wajumbe wa bodi itakuwa miaka mitatu lakini wanaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine cha miaka mitatu tu.

Mwenyekiti ambaye ni Jaji wa mahakama kuu ya Tanzania atakayeteuliwa na waziri husika akisaidiana na Jaji Mkuu
Mwanasheria Mkuu au mwakilishi wake mwenye cheo si cha chini ya Afisa Sheria
Mwakilishi mmoja kutoka jukwaa la taifa la haki jinai
Mwakilishi mmoja kutoka Chama cha Mawakili wa kujitegemea Tanganyika
Mkurugenzi wa huduma za sheria kutoka wizara inayohusika na tawala za mikoa na serikali za mitaa au mwakilishi wake
Mwakilishi wa watu wanaoishi na ulemavu
Mwakilishi mmoja kutoka taasisi zinazowakilishi wasaidizi wa kisheria
Katibu wa Bodi ya taifa ya ushauri wa msaada wa sheria atakuwa ni msajili

Miongoni mwa majukumu ya bodi,Kutoa miongozo ya kisera, kutoa ushauri, Kupitisha ripoti za mwaka za watoa huduma ya msaada wa sheria na kupokea na kutoa maamuzi ya rufani zitakazo pitia maamuzi ya msajili wa watoa huduma za msaada wakisheria.

(b)Ofisi ya msajili wa watoa huduma wa msaada wa kisheria.

(c)Katika ngazi ya taifa kutakuwa na msajili na katika ngazi ya wilaya na mkoa kutakuwa na wasajili wasaidizi. Miongoni mwa kazi zao itakuwa ni pamoja na; Kusajili watoa huduma wa msaada wa kisheria, Kuchunguza malalamiko yote yanayohusiana na watoa huduma ya msaada wa kisheria, Kusimamisha au kufuta usajili wa mtoa huduma ya msaada wa kisheria,kutunza kumbukumbu ya orodha ya watoa huduma ya msaada wa kisheria, Kukagua ofisi za watoa huduma ya msaada wa kisheria ikiwa ni pamoja na kujiridhisha na aina na ubora wa huduma zitolewazo, kutoa elimu ya sheria na ufahamu miongoni mwa wanajamii,aidha, wataratibu na kuwezesha utayarishaji wa mitaala ya kufundishia wasaidizi wa kisheria kwa kushirikisha wadau muhimu.

Read More